Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Uhusiano kati ya Mkurugenzi wa halmashauri, Mkuu wa wilaya

18050 Pic+mkugenzi TanzaniaWeb

Wed, 19 Sep 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Tumeshuhudia kutoelewana kati ya baadhi ya wakuu wa wilaya na wakurugenzi wao. Pia, wakati mwingine kuna magomvi kati ya mwenyekiti wa halmashauri na wakuu wa wilaya au wakurugenzi. Ikitokea viongozi hawa wakawa wanatoka vyama vya siasa tofauti, hali inakuwa mbaya zaidi. Jambo hili tunaliacha kuendelea bila kulitolea ufumbuzi na ikitokea likawa miongoni mwa viongozi vijana: Sote tunajua kwamba taifa letu litajengwa na vijana; matumaini yetu yote na uhai wa taifa letu la leo, kesho na vizazi vijavyo yako mikononi mwa vijana wetu. Ni muhimu vijana hawa kuzingatia sheria, taratibu na miongozo ya uongozi ili kuboresha uongozi wa taifa letu na kupanda matumaini mapya kwenye taifa letu.

Watoto wetu, wanaona yanayotendeka! Wakigombana mkuu wa wilaya na mkurugenzi na kurushwa na vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, tunakuwa tunawafundisha nini watoto wetu. Ni kitu tunafundisha? Ni matumaini yapi tunayapandikiza miongoni mwa watoto wetu na taifa la kesho? Tusiwe wabinafsi, kwa kuangalia maisha yetu ya leo, ni muhimu pia kufikiria Tanzania ya kesho!

Katika ngazi ya wilaya, kuna viongozi watatu wazito. Mkuu wa wilaya, mkurugenzi na mwenyekiti wa halmashauri. Na mara nyingi wananchi wanachanganyikiwa kutofautisha nafasi na umuhimu wa kila mmoja katika nafasi yake. Daima swali linakuwa ni nani kati yao mwenye madaraka makubwa zaidi ya mwingine na je, ni nani kati yao watatu anawajibika kwa nani? Je, hawa wanafanya kazi vipi bila migongano? Je, hawa wanaimarisha serikali za mitaa? Je, wananchi wanafahamu tofauti na umuhimu wa kila mmoja? Je, wao wanafahamu nafasi zao na wajibu zao bila kuingilia mwingine?

Serikali ya awamu wa nne, ilifanya jitihada kubwa kuendesha semina elekezi, ili kuondoa utata huu. Mfano, mwezi wa nane 2006, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kule Dodoma, iliendesha mafunzo ya awali ya wakurugenzi wapya wa halmashauri. Kati ya yale yaliyofundishwa ni uhusiano kati ya mkurugenzi wa halmashauri, mkuu wa wilaya na mwenyekiti/meya wa halmashauri. Bahati mbaya semina hizi zinafanyika kwa viongozi tu! Wananchi hawajapata mafunzo haya, ingawa ni muhimu pia na wao kufahamu mambo mbalimbali yanayohusu serikali za mitaa. Hivyo, lengo la makala hii ni kuwamegea wananchi baadhi ya mambo muhimu katika serikali zao za mitaa. Na leo ninawamegea uhusiano kati ya mkurugenzi wa halmashauri, mkuu wa wilaya na mwenyekiti/meya wa halmashauri. Ninabaki na matumaini kwamba siku za mbele Serikali itafanya mpango wa kuendesha semina kwa wananchi, hasa kwenye ngazi ya Vijiji na Mitaa, ili kuwaelimisha juu ya mambo mbalimbali ya serikali za mitaa.

Pia, ni matumaini yangu kwamba kwa vile sasa hivi migongano hii imejitokeza kwa nguvu. Kuna ulazima wa Serikali kurudi tena mfumo huu wa semina elekezi, kuwafundisha viongozi vijana juu ya mfumo wa utawala na uongozi katika ngazi ya wilaya. Kuna ngazi nyingi za utawala na uongozi, lakini leo nimeanzia kwenye wilaya, maana ngazi hii imeonyesha kuwa na migongano mingi. Ni ngazi ya utawala na uongozi ambayo viongozi na wananchi wanahitaji semina na mwongozo juu ya mfumo huu.

Majukumu ya msingi ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni pamoja na kudumisha amani na usalama baina ya raia wake, kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii na kutoa huduma bora kwa wakazi wake. Na hili, kama anavyosema kila mara Rais John Magufuli, hayana vyama. Ni kwa Watanzania wote. Na hili lisisemwe tu kama wimbo, bali liingizwe kwenye matendo. Kwa kiasi kikubwa, jukumu la kuwaendeleza watu kiuchumi, kijamii na kuwapa huduma bora, limepewa Serikali za mitaa. Katika ngazi ya wilaya, ndiyo mahali ambapo sera na majukumu ya Serikali yanayolenga katika kuwahudumia wananchi zinatekelezwa. Kwa maana nyingine, ngazi hii ina umuhimu wa pekee katika kuhakikisha kuwa majukumu haya yanafanikiwa. Mkuu wa wilaya ndiye mwakilishi wa Rais na mtendaji mkuu wa Serikali kuu ambapo mtendaji mkuu katika halmashauri ni mkurugenzi wa halmashauri. Meya/ mwenyekiti wa halmashauri ni kiongozi wa kisiasa na kiungo cha wawakilishi wa wananchi.

Sheria za nchi zimebainisha majukumu ya Serikali kuu na yale ya Serikali za mitaa katika ngazi hii ya wilaya. Ni muhimu kila upande ukatoa ushirikiano ili kuiwezesha sheria kuchukua mkondo wake katika hali ya amani na ushirikiano. Mfano, uwezo wa mkuu wa wilaya kwa mujibu wa sheria za Serikali za mitaa, uko kwenye sheria Na.19 ya G.A. at District Level Part III (Pg 407), Sheria Na.8 ya 1982 kifungu Na. 78A na kanuni za kudumu za halmashauri.

Pia, kuna uhusiano kwa mujibu wa miongozo ya kiutawala. Kuna mwongozo wa namna ya kuchukua hatua za nidhamu kwa watumishi wanaofanya kazi katika mamlaka za Serikali za mitaa (Barua Na. AB.110/112/01 ya tarehe 12.05.06).

Para 4.1.1 “ Pale halmashauri inapomtuhumu mtumishi anayefanya kazi katika halmashauri na ambaye mamlaka yake ya nidhamu sio halmashauri, mwenyekiti wa halmashauri anatakiwa kuwasilisha tuhuma hizo kwa mkuu wa wilaya ambamo halmashauri hiyo imo na mkuu wa wilaya atamjulisha mkuu wa mkoa haraka iwezekanavyo.”

Licha ya viongozi hawa wawili kuongozwa na sheria katika uhusiano wao, busara na hekima zinawataka kujenga ushirikiano mwema kati yao kwa vile malengo tarajiwa ya sehemu wanazoziongoza zinalenga wananchi walewale wa eneo wanalofanyia kazi. Na hapa neno la kuzingatia ni “ hekima na busara”. Uwazi na uwajibikaji kwa pande zote mbili ukiambatana na kuheshimiana utaweka mazingira mazuri kwa utekelezaji wa majukumu yao.

Maeneo ambayo yanaweza kusababisha uhusiano mbaya kati ya mkurugenzi wa halmashauri na mkuu wa wilaya ni pamoja na:-

-Serikali za mitaa zimepewa madaraka ya kujiamulia mambo yake wenyewe bila ya kuingiliwa ili mradi sheria na miongozo ya kitaifa inafuatwa. Eneo hili limekuwa likitafsiriwa vibaya na baadhi ya wakurugenzi kwa kufanya maamuzi ambayo hayana tija kwa halmashauri;

-Kwa upande wao wakuu wa wilaya wamekuwa na shauku kubwa kama wakuu wa Serikali na wawakilishi wa Rais ya kuhakikisha kwamba halmashauri zao zinafanikiwa katika kutekeleza majukumu yake;

-Serikali kuu kutopeleka fedha na vitendea kazi vya kutosha kwa wakuu wa wilaya na hivyo kuzifanya ofisi zao kuwa tegemezi/ombaomba kwa wakurugenzi wa halmashauri na hivyo kushindwa kutekeleza ipasavyo majukumu yao. Hali hii inashusha hadhi ya mkuu wa wilaya mbele ya mkurugenzi;

-Kukosekana kwa taratibu za wazi za kiutawala za maandishi zinazoongoza mahusiano baina ya viongozi hawa. Mara nyingi viongozi hawa wamekuwa wakiongozwa kwa njia ya muafaka ziadi kuliko taratibu zilizowekwa.

Ili kuhakikisha kuwa kuna mahusiano mazuri kati ya mkuu wa wilaya na mkurugenzi wa halmashauri ni lazima kuzingatia yafuatayo :-

-Kila upande uhakikishe unatekeleza majukumu yake ipasavyo kwa manufaa ya wananchi kwa kuzingatia Sheria, kanuni na taratibu zilizopo;

-Serikali kuu iziimarishe Ofisi za Wakuu wa Wilaya kwa kuzipa fedha na nyenzo za kutosha ili kumwezesha mkuu wa wilaya kutekeleza majukumu yake ya kiserikali;

-Jitihada zifanywe za Kutoa miongozo ya maandishi inayobainisha nani afanye nini katika masuala ya kiutawala na

-Kila upande uweke mazingira mazuri ili kumwezesha mwenzake kutekeleza majukumu yake.

Kwa upande wa majukumu ya msingi ya mwenyekiti/meya ni kama ifuatavyo :- Yeye ndiye mwenyekiti wa baraza la madiwani. Kikao cha baraza la madiwani ni kikubwa kuliko vikao vyote katika halmashauri; Ni kiongozi mkuu wa kisiasa wa halmashauri; Ni kinara wa sherehe za halmashauri na yeye ndiye hutoa taarifa kwa wananchi kuhusu utekelezaji wa shughuli za halmashauri mwishoni mwa kila mwaka akionyesha shughuli zilizotekelezwa, mafanikio na matatizo yaliyojitokeza.

La kukumbuka ni kwamba meya/mwenyekiti si mfanyakazi wa halmashauri. Mfumo wa Serikali za mitaa uliopo hapa nchini hauruhusu meya/mwenyekiti wa halmashauri, wala diwani yeyote kuwa na madaraka ya kiutendaji (Tazama Kanuni za Maadili ya Madiwani aya ya 25 na 27). Ni watumishi na wala si madiwani wanaotekeleza.

Ili kudumisha uhusiano mwema kati ya meya/mwenyekiti na mkurugenzi wa halmashauri, meya/ mwenyekiti asijihusishe na shughuli za utendaji kazi wa kila siku. Ni kwa sababu hii na sababu nyinginezo za kiuchumi, wizara yenye dhamana ya Serikali za mitaa ilielekeza wenyeviti na mameya wawe ofisini siku mbili kwa wiki ili kupunguza migongano.

Uhusiano mzuri na thabiti kati ya viongozi hawa watatu (Mkuu wa wilaya, mwenyekiti/meya wa halmashauri na mkurugenzi wa halmashauri) ni nyenzo na hitaji muhimu siyo tu kwa amani na utulivu katika wilaya, bali kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya wilaya na halmashauri husika. Hivyo ni muhimu kabisa kuwa na mahusiano mazuri kati yao.

Padri Privatus Karugendo.

+255754633122

[email protected]

Chanzo: mwananchi.co.tz