Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Ufugaji samaki vizimbani waongeza tija

F78c720f2475c551cda0a9a3916a932f Ufugaji samaki vizimbani waongeza tija

Wed, 5 Aug 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

TEKNOLOJIA ya ufugaji samaki kwa kutumia vizimba katika Ziwa Victoria umeonesha matokeo mazuri huku wafugaji wakihimizwa kujiunga kwenye vikundi, kupewa mafunzo.

Akizungumza kwenye maonesho ya wakulima yanayoendelea katika viwanja vya Nyakabindi mkoani Simiyu, Ofisa Uvuvi kutoka Idara ya ukuzaji viumbe maji ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Oscar Mashiranga alisema hadi sasa kuna jumla ya vizimba 431 vyenye samaki katika ziwa hilo.

Mashiranga alisema ufugaji wa samaki kwa kutumia vizimba katika ziwa hilo umeanza kueleweka kwa wananchi na kwamba teknolojia hiyo ilianza kutolewa nchini mwaka 2016 baada ya utafiti kufanywa na Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi (Tafiri) wa kutafuta njia bora za ufugaji samaki.

Alisema ufugaji samaki kwa kutumia vizimba una faida kwa sababu kizimba kimoja chenye ukubwa wa mita tano upana kwa mita tano urefu na kina cha mita nne, kina uwezo wa kufuga samaki 10,000 ambao wakifugwa vizuri na kuuzwa baada ya miezi sita, mfugaji hupata faida nzuri.

“Ufugaji samaki kwenye vizimba katika Ziwa Viktoria una matokeo mazuri, wafugaji walioanza kufuga wanapata faida kwa sababu eneo dogo linafuga samaki wengi,” alisema.

Akizungumzia vizimba, Mashiranga alisema samaki huwekwa kwenye uzio uliotengenezwa kwa nyavu unaoelea majini na kuruhusu maji kuingia na kutoka kwa ajili ya hewa na kutoa uchafu.

Akisema baada ya teknolojia hiyo kuanzishwa mwaka 2016 wafugaji wachache walioelimishwa walikubali kuanza kufuga na jumla ya vizimba 109 vilijengwa na hadi sasa vimeongezeka hadi kufikia 431.

“Ufugaji wa masaki kwa vizimba ni njia mpya na yenye tija kwa sababu ya mazao mengi yanayozalishwa, ingawa mwanzo kuna gharama za kuanzisha mradi huo lakini faida nzuri huanza kuonekana kwenye mavuna ya pili na kuendelea,” alisema.

Akizungumzia elimu aliyopata kwenye banda hilo, Joseph Mabula alisema anapenda kufuga samaki lakini changamoto mtaji wa kuanzisha bwawa la kufugia ambapo Mashiranga aliwashauri kujiunga kwenye vikundi ili kupunguza gharama.

Chanzo: habarileo.co.tz