Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Ubungo waandamana kwa DC kudai maji

Bongo Dsm Maji.jpeg Ubungo waandamana kwa DC kudai maji

Mon, 14 Nov 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wakazi wa eneo la Luguruni Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salaam wameandamana hadi ofisi ya mkuu wa wilaya ya Ubungo (DC), Kheri James kudai huduma ya maji waliyoikosa kwa miezi mitatu sasa huku wakiletewa bili.

Wakazi hao wakiwa wamebeba ndoo zao zikiwa tupu walikuwa wakiimba nyimbo mbalimbali zilizokuwa zikiashiria kuwa wanahitaji maji huku wanawake wakiziweka kichwani na kumtaka mkuu wa wilaya hiyo kuwatua ndoo.

George Ngao ambaye ni mmoja wa wananchi katika eneo hilo amesema licha ya mgao wa maji uliopo lakini wao hawajapata maji kwa miezi mitatu sasa.

“Mbaya zaidi tunalipishwa bili za maji, pia maji haya tunayoyataka yanapita katika eneo letu, mitaa mingine yanakokwenda wanapata maji ila sisi hatuna.”

“Tumejitahidi kutafuta suluhisho bila mafanikio mwisho tumeamua kuja kwa mkuu wa wilaya atupe suluhu ya suala hili,” amesema

Kilio cha wakazi hawa kinakuja ikiwa ni baada ya kuwapo kwa mgao wa maji ndani ya jiji la Dar es Salaam uliotokana na kupungua kwa uzalishaji maji katika mto Ruvu ambao ndiyo chanzo kikuu cha maji kinachotegewa.

Scholastica Mwenda ambaye pia ni mkazi wa eneo hilo amesema kwa miezi hiyo mitatu walilazimika kununua dumu 1 kwa Sh1000 kwa maji ya bomba huku maji ya chumvi kwa Sh500.

“Kwa walioweza kutafuta kwa kichwa kwenye visima walifanya hivyo, ilifika hatua bajeti zetu za chakula zinachukuliwa maji, hata watoto kujisaidia unawapangia kwa sababu maji hakuna, vyoo vipo ndani nyumba itanuka,” amesema

Anasema athari yake ni magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu huku akieleza hata maji ya kununua wanayotumia wakati mwingine hawajui vyanzo vyake na hata usalama wa vyombo vinavyotumika katika kubeba.

Hata hivyo, bado anasisitiza kuwa hakuna mwananchi wa kawaida anayeweza kununua maji ya Sh10,000 kwa siku kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

“Ukitaka kufua na kufanya usafi wa nyumba maji mengi yanatumika, kuoga mara moja kwa kutwa na makopo ya kuhesabu, sasa hili ni mimi ambaye nina familia ya watu watatu lakini jirani yangu ana familia ya watu 12 unaweza kuona wanaishije humo ndani.

Akizungumzia suala hilo mkuu wa wilaya ya Ubungo, Kheri James aliwahidi wananchi hao kuwa watapata huduma ya maji leo.

“Kuanzia 7:45 mchana kazi yangu itakuwa ni kupita na kuangalia maji yanatoka wapi na wapi hakuna maji, tuheshimu ratiba ya mgao wa maji tuliyoitoa, mnatekelezaje, Wananchi tumeshawaandaa kuwa tatizo lipo na hicho kidogo tutakigawana kwa mgao,” James.

Amesema inashangaza kukuta baadhi ya maeneo barabarani maji yanamwagika lakini Wananchi hawapati maji.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live