Dar es Salaam. Benki ya UBA Tanzania imetoa vitabu vya fasihi simulizi katika shule mbalimbali za Sekondari ili kupunguza uhaba wa vitabu katika shule hizo.
Miongoni mwa shule zilizopatiwa msaada wa vitabu hivyo ni pamoja na ya Sekondari ya Ugombolwa, Miombani na Shule ya sekondari ya Zawadi.
Lengo la msaada huo limeelezwa kuwa ni kuongeza ufahamu kwa wanafunzi.
Vitabu hivyo ambavyo ni vya Things fall apart, The fishermen, The girl that can pamoja na Fine Boy kutoka kwa waandishi maarufu akiwamo Chinua Achebe na Chigozie Obioma.
Akizunguza leo Jumanne Septemba 3, 2019 jijini Dar es Salaam, Mkuu wa kitengo cha digitali cha Benki ya UBA, Asupya Nalingigwa amesema msaada huo unakwenda kusaidia ukuaji wa elimu nchini Tanzania.
Amesema ofisi yake imejipangia utaratibu wa kugawa vitabu kwenye shule za sekondari kila mara pamoja na kuwezesha miundo mbinu mbalimbali ya sekta ya elimu.
Pia Soma
- Bei mafuta ya petroli, dizeli yapanda Tanzania
- Kesi ya DC Chemba: Ulimuoa mkiwa vijana, leo uzeeni unataka kumuacha ili aolewe na nani
- Mchungaji, wake zake wawili wapandishwa kortini Dar
“Someni sana vitabu, faida zake ni nyingi kuliko kujikita kwenye mambo yasiyo ya muhimu kwenye mitandano ya kijamii,” amesema Nalingiwa.
Amewaasa kuitumia mitandao hiyo kwa kujisomea zaidi na kujifunza mambo mbalimbali yenye tija.
Akizungumza kwa niaba ya wenzake wakati anapokea msaada huo, Mkuu wa Shule ya Sekondari Ugombolwa, Simon Machia ameishukuru benki hiyo kwa msaada huo na ametoa wito kwa wanafunzi kutumia vitabu hivyo kwa makini ili UBA baadaye ije ione faida ya msaada wake kwao.
Ametoa wito kwa wadau wengine kujitokeza kuwasaidia katika maeneo mengine aliyoyataja kama madarasa, viti, meza, madawati na kompyuta.