Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Tulila; kivutio kipya cha utalii mkoani Ruvuma

Fa2fe596a80301b9ea6cbede73078f6b Tulila; kivutio kipya cha utalii mkoani Ruvuma

Fri, 21 May 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

TULILA ipo katika kata ya Mpepai Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma ambako kumegundulika kuwa vivutio vya kipekee vya utalii na uwekezaji.

Hata hivyo maporomoko ya Tulila ndipo kuna mradi wa umeme wa maji toka maporomoko ya mto Ruvuma, unaomilikiwa na watawa wa Benedictine wa Mtakatifu Agnes Chipole Jimbo kuu la Songea.

Mradi huu unazalisha megawati tano ambazo zilimaliza tatizo la umeme katika mji wa Songea kabla ya Mkoa wa Ruvuma kuingizwa katika grid ya Taifa.

Kutoka Songea mjini hadi Tulila ni takribani kilometa 89. Kivutio hiki bado hakifahamiki na wengi ni eneo lenye mandhari nzuri ya kuvutia na mtu unaweza kufanya utalii wa kupiga picha, kuogelea, kuendesha mtumbwi pia kuna fukwe nzuri za mto Ruvuma.

Uchunguzi wa mwandishi umebaini kuwa bwawa la kuzalishaji umeme lenyewe pekee ni kivutio tosha cha utalii wa majini na katika eneo hili kuna aina adimu za ndege ambao ni kivutio pia.

Utalii ambao unaweza kushamiri hivi sasa katika Mkoa wa Ruvuma na Taifa kwa ujumla ni utalii wa ndani ambapo katika eneo la Tulila watawa wanamiliki eneo lenye ukubwa wa ekari 1000.

Watawa katika eneo la bwawa wamewekeza kwenye ufugaji wa samaki wa aina mbalimbali na kupanda miti aina ya mitiki yenye thamani kubwa kwa sababu ekari moja ya mitiki inaweza kumuingizia mkulima hadi shilingi milioni 400.

Afisa Maliasili na Utalii Mkoa wa Ruvuma, Afrikanus Challe anasema katika uchunguzi wao umebaini kuwa samaki hao wanavutia makundi ya ndege wakiwemo tai ambao wanakula samaki.

Watawa hao wanafuga mbuni, bata mzinga na aina nyingine za ndege ambao ni kivutio unapokuwa katika eneo Tulila.

Maporomoko ya Tulila yapo kilometa sita toka Pori la Akiba la Liparamba lenye wanyama wa aina mbalimbali hivyo watalii watakaotembelea Liparamba wanaweza kufika kwenye maporomoko ya Tulila ambako wanaweza kupata malazi na chakula kwenye hoteli za kisasa za kitalii zinazomilikiwa na watawa hao.

Inaelezwa kwamba tembo wa Liparamba pia wanafika kwenye maporomoko ya Tulila na kwamba majira ya asubuhi na jioni makundi makubwa ya ndege na viboko hufika pia katika eneo hilo kunywa maji na kula chakula.

Mto Ruvuma ambao chanzo chake ni milima ya Matogoro iliyopo nje kidogo ya mji wa Songea, ni miongoni mwa mito maarufu barani Afrika ukimwaga maji yake Bahari ya Hindi .

Mwandishi ni Ofisa Habari Mkoa wa Ruvuma

HYPERLINK "https://web.facebook.com/photo.php?fbid=1066628616804746&set=pcb.1066629186804689&type=3&__tn__=HH-R&eid=ARBzL0dAau1epc-KYEOkGVsaOfrxs--hROZ4PCoj7X0a_FRRGBF005hC1sqFlAsKJKgVGKxwj4WTb55R"

Chanzo: www.habarileo.co.tz