Dar es Salaam. Meya wa Manispaa ya Temeke jijini Dar es Salaam, Abdallah Chaurembo amewataka wananchi kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya ili kujikinga na ugonjwa wa corona.
Ametoa kauli hiyo leo Jumatano Aprili 15, 2020 wakati akipokea vitakasa mikono, barakoa na glovu kutoka kampuni ya General Petroleum.
Chaurembo amesema wananchi wafuate maelekezo ya wataalamu kwa kuwa Temeke ni moja ya manispaa zenye wagonjwa wa corona.
"Msaada huu umekuja wakati muafaka kwa ajili ya wananchi wa Manispaa ya Temeke. Vifaa hivi vimesambazwa kwenye hospitali ya rufaa ya Temeke na hospitali ya Wilaya ya Mbagala Zakiem pamoja na kata zote 23 za manispaa, pia tuendelee kuchukua tahadhali kama Serikali inavyotutaka,” amesema Chaurembo.
Pia Soma
- Hakimu amtaka Shamimu Mahakamani
- Mahakama yataka uchunguzi kesi ya Tito wa LHRC kukamilika
- Sh130 bilioni za malimbikizo ya mshahara ya watumishi Tanzania zalipwa tangu 2015
- Polisi wazungumzia vifo vya mahabusu, mfungwa jijini Mwanza
Mganga Mkuu wa Manispaa ya Temeke, Dk Gwamaka Mwabulambo amesema wananchi wanatakiwa kufahamu kuwa ugonjwa huo hauna tiba na wachukue tahadhari kwa kuepuka msongamano na kushikana kwa mikono.
Ofisa rasilimali watu wa kampuni hiyo, Aboubakar Kondo amesema wametoa msaada wa barakoa 1200, glovu 1200 na vitakasa mikono 1000.
Kondo amesema kampuni hiyo imeunga mkono Serikali kupambana na maambukizi ya corona na hawataishia Temeke watafanya hivyo katika wilaya za Ilala Kinondoni na Ubungo.