Arusha. Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamis Kigwangallah amezindua mpango wa kuwafunga tembo vifaa vya mawasiliano ya kijiographia (GPS) ili kuweza kuwafuatilia na kuzuia ujangili na kuvutia watalii zaidi.
Waziri Kigwangallah ambaye jana alishiriki mapokezi ya watalii 343 kutoka China, amesema lengo la Serikali kwa sasa ni kuendelea kuboresha uhifadhi hasa bada ya ongezeko kubwa la tembo na hivyo kuvutia watalii zaidi.
"Vifaa hivi vya GPS vitawawezesha tembo kufuatiliwa mienendo yao na hivyo kuweza kudhibiti matukio ya tembo kuvamia mashamba na masuala ya ujangili kwani pia kutawekwa uzio wa kielekroniki," amesema.
Waziri Dk Kigwangallah aliipongeza taasisi ya Friedkin Conservation Fund (FCF) kwa kufadhili mradi huo na Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori (Tawiri) kwa kuendesha zoezi hilo.
Mkurugenzi wa FCF, Nicholas Negri amesema mradi huo utasaidia sana uhifadhi nchini na kuvutia watalii zaidi.
Alisema FCF itaendelea kushirikiana na Serikali katika kuendeleza uhifadhi kwani pia tayari wamefadhili mradi wa kuwafunga vifaa vya mawasiliano faru ili kuwalinda na ujangili.
Pia Soma
- Serikali kuikatia rufaa hukumu ya wakurugenzi kusimamia uchaguzi
- Serikali yachukua hatua ndege zake kuchelewa kuanza safari
- Serikali ya Tanzania yatoa neno ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo
Amesema katika eneo la hifadhi ya jamii ya makao na pori la akiba la Maswa, tembo 18 watafungwa vifaa vya GPS.
Mtafiti wa Tawiri, Dk Emmanuel Masenga amesema hadi sasa tembo 95 wamefungwa mikanda ya GPS katika maeneo mbalimbali ya hifadhi nchini.