Changamoto ya ukosefu wa milango na madawati ya kutosha katika shule za sekondari wilayani Muheza mkoani Tanga nchini Tanzania imeanza kupatiwa ufumbuzi baada ya mbao 184 kutolewa kwa ajili ya kazi hiyo.
Mbao hizo zenye thamani ya Sh4.6 milioni zimetolewa leo Jumamosi 13, 2019 na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kupitia shamba lake la miti la Lunguza lililopo wilayani humo.
Kaimu Meneja wa shamba hilo, Elneema Mwasalanga amesema wametoa mbao hizo ili kuwezesha upatikanaji wa madawati na kuhakikisha wanafunzi wanasoma katika madarasa bora.
Amesema jamii iliyo jirani na shamba la Lunguza ina haki ya kupata matunda ya shamba hilo na ndiyo sababu uongozi umeona ushiriki katika kutatua changamoto ya madawati.
“Serikali imekuwa ikifanya jitihada kuhakikisha elimu inatolewa bure katika mazingira bora ndiyo maana na sisi tumeona tutoe mbao ili kupunguza uhaba wa madawati katika shule za sekondari zilizopo Muheza,”
“Elimu ndiyo pekee ambayo inaweza kutuboreshea namna ya uelewa katika uhifadhi na uzalishaji, vijana wakisoma wataelewa umuhimu wa uhifadhi wa mazingira na watasaidia katika kuelimisha jamii ili misitu iendelee kuwepo,”
Pia Soma
- Wakulima sasa kucheka kupatikana kwa tiba ya muhogo mnyauko
- Kilimo cha Pareto kilivyompa utajiri Wema
- Watanzania watatu wauawa shambulizi la al- Shabab nchini Somalia