Mbozi. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Songwe imebaini udanganyifu wa zaidi ya Sh200.9 milioni katika mradi wa maji Iyula wilayani Mbozi.
Hayo yameelezwa leo Jumanne Aprili 14, 2020 na kamanda wa Takukuru mkoani Songwe, Damas Suta wakati akiwasilisha taarifa ya taasisi hiyo katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita.
Amesema udanganyifu umefanyika katika ununuzi wa vifaa kwa kuongeza bei ya kila kifaa, akibainisha kuwa kasoro zaidi imekutwa katika ununuzi wa nodno.
Amebainisha kuwa mradi huo wa zaidi ya Sh5.1 bilioni ulianza kutekelezwa mwaka 2017, wakati huo zilihitajika nondo za ujazo wa milimita 10 zilizokuwa zikiuzwa Sh7,800 lakini mkandarasi aliandika alinunua kwa Sh78, 000.
Amesema mkandarasi huyo ambaye ni kampuni ya STC Construction ya Dar es salaam alifanya kitendo hicho kutokana na uzembe wa aliyekuwa mhandisi wa halmashauri ya Mbozi pamoja na wataalamu wengine walioshiriki kufanya tathmini ya zabuni hiyo kwa makusudi.