Mbeya. Serikali imeagiza taasisi zote za umma nchini kuanzisha vikundi vya kuhifadhi na kulinda mazingira kwa lengo la kuhakikisha maeneo yanayozunguka taasisi hizo na jamii yanakuwa salama.
Agizo Hilo limetolewa leo Alhamisi Novemba 29, 2018 Kyela mkoani Mbeya na naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Musa Sima wakati akizingumza na vikundi vya uhifadhi mazingira na watumishi wa halmashauri za mikoa mitatu ya Mbeya, Njombe na Ruvuma.
Mikoa hiyo inatekeleza Mradi wa usimamizi endelevu wa rasilimali ardhi kati Ukanda wa Ziwa Nyasa (SLM).
Sima amesema ili kuendelea kukabiliana na changamoto ya uharibifu wa mazingira ni lazima kila taasisi ioteshe miche ya miti kuzunguka maeneo husika.
Ameagiza wakurugenzi wa halmashauri zote kuhakikisha wanapeleka wataalamu wao shuleni watakaosaidiana na walimu na wanafunzi kuotesha miti kwa kila shule, kwamba mpango huo utakuwa endelevu.
“Na katika hili niwatake wakuu wa wilaya, wakurugenzi kuhakikisha idara zote zilizopo kwenye halmashauri zenu ikushirikiana na waliojitoa kupigania mazingira,” amesema.
Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Claudia Kitta amemueleza naibu waziri huyo kwamba katika wilaya yake bado kuna changamoto ya uharibifu wa mazingira kutokana na shughuli za kibinadamu.
Mratibu wa mradi wa SLM, Michael Mwankupili amesema mradi unatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo na utakamilika mwaka 2020.
Amesema mradi huo umejikita zaidi katika shughuli za kutunza na kuhifadhi mazingira ukanda wa ziwa Nyasa.