Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema mvua zinazoendelea kunyesha ukanda wa Pwani zitamalizika leo Jumanne Septemba 10,2019.
Imesema mvua hizo ni za kawaida ambazo zinatoka nje ya msimu kutokana na mabadiliko ya muda mfupi ya mifumo ya hali ya hewa.
Meneja wa kituo kikuu cha utabiri cha mamlaka hiyo, Samuel Mbuya akizungumza jana Jumatatu Septemba 9, 2019 na Mwananchi alisema mvua hizo zinatawaliwa na upepo wa kusi ambao unaleta hewa ya baridi.
Mbuya alisema hali ya joto la bahari ya Hindi ukanda wa Afrika Mashariki limeongezeka kuanzia Agosti 2019 ambapo inabadilisha upepo wa Kusi na unabeba hali ya joto katika maeneo ya Pwani ya Mashariki na kusababisha mvua hizo zinazoendelea kunyesha.
Alisema mvua hizo zitanyesha katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Tanga na Visiwa vya Unguja na Pemba, Zanzibar
“Mvua hizi zinazonyesha siyo za vuli zinatoka nje ya msimu ni mabadiliko ya mifumo ya hali ya hewa na zitaendelea hadi kesho (leo),” alisema Mbuya.
Pia Soma
- Anayepumulia mashine afungiwa umeme, alia na gari la wagonjwa
- Tira yazitaka kampuni za bima kuwafuata wenye kipato kidogo
- VIDEO: Mahakama yamhukumu mchungaji na wake zake kwenda jela, kulipa faini
Mbuya alisema kuanzia leo Jumatatu hadi Septemba 9 hadi Septemba 11, 2019 kutakuwa na upepo mkali katika mikoa hiyo.
Alisema uwezekano wa kutokea athari ni mkubwa kwa upande wa usafiri wa majini, kuathirika kwa shughuli za uvuvi na ugumu wa upatikanaji wa samaki
“Ninawashauri watumiaji wa bahari maeneo ya Ziwa Nyasa, Victoria na Tanganyika na wachukue tahadhali na hatua stahiki hivyo tutaendelea kufuatilia hali hii na itatoa mrejeo kila itakapobidi,” alisema.