Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Deogratius Ndejembi amemwagiza Kamanda wa TAKUKURU wilayani Ruangwa kufanya uchunguzi wa matumizi ya kiasi cha shilingi 102,080,357.14 zilizotolewa na Serikali kupitia TASAF ili kujenga zahanati ya Kijiji cha Mtakuja na kuwasilisha taarifa ya uchunguzi huo kwake kabla ya kuhitimisha ziara yake mkoani Lindi.
Ndejembi ametoa maelekezo hayo baada ya kukagua na kutoridhishwa na utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa zahanati ya Kijiji cha Mtakuja, akiwa kwenye ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini unaoratibiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).
Amesema hajaridhishwa na taarifa ya ujenzi huo kutokana na mapungufu yaliyomo ikiwa ni pamoja na kiasi cha Tsh. Milioni 27 tu zilizobaki kwenye akaunti kati ya Tsh. milioni 102 zilizotolewa na TASAF, hivyo hakitoweza kukamilisha ujenzi wa zahanati hiyo.
Kutokana na mapungufu yaliyobainika Waziri Ndejembi amemuelekeza Kamanda wa TAKUKURU kuhakikisha anafanya uchunguzi maalum na kumchukulia hatua yeyote akatayebainika kuhusika na ubadhirifu wa fedha za umma.