TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Singida imeokoa zaidi ya Sh milioni 136 katika kipindi cha Aprili hadi Juni mwaka huu.
Akizungumza mjini Singida, Mkuu wa Takukuru mkoa wa Singida, Adili Elinipenda alisema kuwa fedha zilizookolewa zilitokana na kasoro za kiutendaji kwenye sekta mbalimbali; ikiwemo mikopo ya riba iliyopindukia inayotozwa na wakopeshaji wasio rasmi, wananchi wema kubambikiziwa kesi kisha kupigwa faini na echepushaji wa fedha za umma kwa nia ovu.
Aidha, alieleza kuwa katika kudhibiti mianya ya rushwa kwa kipindi kilichotajwa, Taasisi hiyo ilifanya ufuatiliaji wa miradi ya Maji na Ujenzi wa Karakana ya Mifugo Chuo cha Ufundi Veta Singida na uchambuzi wa mifumo kuhusu udhibiti wa mianya ya rushwa katika utatuzi migogoro ya ardhi kwenye Mabaraza ya Kata na Vijiji wilayani Singida.