Walinzi shirikishi maarufu kama sungusungu, wanadaiwa kumuua kwa kipigo, kijana mmoja mwenye changamoto ya afya ya akili, kwa kumpiga wakimtuhumu kuwa ni mwizi wakati akichota maji usiku.
Inaelezwa kuwa kijana huyo, alipatwa na changamoto ya afya ya akili baada ya kufiwa na baba yake, ambapo alikuwa na kawaida ya kujifungia ndani na kutoka usiku.
Siku ya tukio, inaelezwa kuwa kijana huyo ambaye mama yake anajulikana kwa jina maarufu la Mama Nandy, alitoka usiku kwenda kuchota maji, ambapo alikutana na sungusungu hao ambao baada ya kushindwa kuelewana, walianza kumpiga.
Baada ya kuzidiwa, alipelekwa hospitali na baadaye kufariki, ambapo ndugu zake hawakuwa na taarifa za kilichokuwa kinaendelea, mpaka walipoenda kuukuta mwili wake mochwari, siku nne baada ya tukio.