POLISI mkoani Geita imewakamata watu sita wanaosadikiwa ni majambazi wakidaiwa kumuua Beatrice Silvanusy (29), mfanyabiashara na mkazi wa Mtaa wa Ibolelo, Kata ya Nyankumbu wilayani Geita, Aprili 27, mwaka huu.
Akitoa taarifa hiyo jana mbele ya waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Henry Mwaibambe aliwataja watuhumiwa hao ni Yasini Zuberi (36), Khasimu Marwa (39), Leonard Emmanuel (34), Fikiri Ezekieli (31), Thomas Daniel (29) na Samson Charles (30) wote wakazi wa Wilaya ya Geita.
Kamanda Mwaibambe alisema baada ya tukio, Polisi ilifanya upelelezi wa kina na kuwakamata watuhumiwa hao wakiwa na simu ya marehemu na wamekiri kugawana fedha kiasi cha Sh milioni 1.5 ambayo walimpora Beatrice.
Alieleza kuwa upelelezi wa kesi hiyo umeshakamilika na watuhumiwa walifikishwa mahakamani jana na kusomewa shitaka la mauaji namba 19/2021 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Geita.
Mapema mwezi huu Polisi ilithibitisha kutokea kwa mauaji ya mfanyabiashara huyo usiku wa Aprili 27, mwaka huu majira ya saa nne usiku wakati akiwa anatokea kwenye shughuli zake za biashara kurejea nyumbani.
Polisi ilieleza kuwa wakati Beatrice akiwa kwenye usafiri wa bajaji, alivamiwa na kundi la majambazi zaidi ya watano na kumpiga na kitu kizito kichwani na kupelekea umauti wake ambako walimpora simu na fedha alizokuwa nazo.