Serengeti. Simba 14 waliokuwa wanakula mifugo katika vijiji vya Bukore na Nyichoka wilayani Serengeti wamekamatwa na kuhifadhiwa katika zizi kwa ajili ya kupelekwa maeneo husika.
Kukamatwa kwa simba hao 14 kunafanya jumla ya waliokamatwa kufikia 31.
Mwaka 2019 simba 17 walikamatwa na kupelekwa hifadhi ya Taifa ya Burigi Chato.
Akizungumza leo Jumamosi Machi 21, 2020 mkuu wa Wilaya ya Serengeti, Nurdin Babu amesema awali waliwakamata simba sita na jana nane, “kwa sasa tunasubiri maelekezo ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Kukamatwa kwa familia hiyo ya simba tunaamini wamebaki wawili na watoto ambao wakikamatwa tatizo tunaamini litakuwa limekwisha.”
Ofisa wanyamapori wa Wilaya hiyo, John Lendoyani amesema kundi hilo la simba limewasumbua kwa muda mrefu na walikuwa wakila mifugo.