Serengeti. Unaweza kusema maofisa wanyamapori wamezidiwa ujanja na kundi la simba wanaokula mifugo kila siku katika kijiji cha Kwitete wilayani Serengeti.
Kuanzia Novemba 2019 hadi leo Jumamosi Desemba 21, 2019 simba wamekula mifugo katika vijiji vya Robanda, Nyichoka, Bukore , Nyanungu na Kwitete na kujeruhi watu wawili. Simba mmoja aliuawa kwa kupigwa risasi na askari wa wanyamapori.
Akizungumza na Mwananchi ofisa mtendaji kijiji cha Kwitete kata ya Nyamoko, Makuru Sabarya amesema katika kijiji hicho simba wameua ng'ombe 25, kubainisha kuwa tayari wamejaza fomu kwa ajili ya tathmini ya wananchi ambao mifugo yao imeuawa na wanyamapori hao.
Kata ya Kyambahi zaidi ya ng'ombe 26 wameuawa, mbuzi 49, kondoo 12 na nguruwe mmoja huku kijiji cha Robanda, Samwel Mahewa akidai ng'ombe wake 26 wameliwa.
"Sisi tupo mbali sana na maeneo ya hifadhi, simba wamekuja na kupiga kambi hapa kijiji. Juzi wameua ng'ombe mmoja, leo (juzi) usiku watatu, wakiishaua wanakimbilia mlimani ambako askari hawawezi kufika. Askari wakienda milimani hata wakipiga risasi simba hawatoki, jioni wanakuja tena kwenye mazizi ya ng’ombe,” alisema Mahewa.
Mkuu wa Wilaya ya Serengeti, Nurdin Babu amemuomba mkurugenzi wa wanyamapori kupeleka kikosi cha madaktari wa wanyamapori kuwapiga simba hao risasi za ganzi ili wawahamishe ili kuepusha madhara zaidi.