Mwili wa aliyekuwa padri wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Mbeya, Michael Samson raia wa Malawi wa shirika la Wamisionari wa Afrika umezikwa leo katika makaburi ya kanisa hilo yaliyopo Mwanjelwa jijini Mbeya.
Katika mazishi hayo, viongozi mbalimbali wa dini wakiwemo kutoka Malawi wameshiriki mazishi huku kilio chao ikiwa ni kufanywa uchunguzi kuwabaini waliohusika na mauaji hayo ya kikatili.
Akizungumza kabla ya maziko mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera amesema tayari ameelekeza Jeshi la Polisi kufanya doria ya mara kwa mara katika maeneo ya viongozi wa dini kuhakikisha usalama.
Amesema tukio hilo limewashtua kwani ni muda mrefu tangu kuripotiwa kwa mauaji ya kiongozi wa dini na kubainisha kuwa amewapa maelekezo kuendelea na uchunguzi kubaini waliohusika.
"Hii ni aibu kubwa kwa mkoa wetu, ni muda mrefu kuwapo matukio kama haya tena kutokea kwa kiongozi wa dini, nimeelekeza Jeshi la Polisi kufanya doria ya mara kwa mara katika maeneo ya viongozi wa dini ambao wanasaidia kuweka amani, lakini kufanya uchunguzi zaidi kuwakamata wahusika," amesema Homera.
SP Halamela Sibula akizungumza kwa niaba ya kamanda wa polisi mkoani humo, Urlich Matei, amesema watahakikisha wanawasaka waliohusika na tukio hilo.
"Niwaombe waumini tupokee msiba huu kiimani, lakini niombe kufuatiliwa waliohusika pengine kukamatwa na haki kutendeka," amesema Mawelera.
Katibu mkuu wa shirika la Wamisionari wa Afrika, Anthony Alkisi amesema walipokea taarifa za msiba huo kwa mshtuko akieleza kuwa marehemu alikuwa mchapakazi na mkarimu akitumia muda mwingi kufundisha na kueneza injili.
"Kwa niaba ya shirika la wamisionari wa Afrika, tunaungana na wafiwa wote katika kipindi hiki kigumu, viongozi wetu wa juu walitamani kushiriki mazishi haya lakini haikuwezekana kwa kuwa wapo katika mkutano mkuu nchini Oman, padri alikuwa mchapa kazi ndio kitu tutaendelea kumkumbuka," amesema Alkisi.