Siha. Barabara yenye urefu wa kilomita 32.2 iliyojengwa kwa kiwango cha lami kutoka Sanya juu hadi Elerai wilayani Siha, Mkoani Kilimanjaro, inatarajiwa kufunguliwa rasmi siku chache zijazo baada ya ujenzi wake kukamilika.
Hayo yamesemwa jana Jumamosi Juni 15 na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira alipofanya ziara ya kukagua barabara hiyo.
Amesema siku chache zijazo barabara hiyo itafunguliwa na kiongozi mkubwa wa Serikali.
“Bara bara hii itafunguliwa rasmi na kiongozi mkubwa wa Serikali na itafungua fursa mbalimbali za bishara katika mkoa wetu, pia Serikali itaimarisha mawasiliano ya mipaka yetu na nchi jirani ya Kenya, hivyo hatutegemei kuona biashara za magendo zikipitishwa katika barabara hii,” amesema Mghwira.
Naye msimamizi wa ujenzi wa mradi huo mkubwa wa barabara ambaye pia ni Meneja wa wakala wa barabara mkoani humo (Tanroad), Mhandisi Nkolante Ntije amesema barabara hiyo yenye urefu wa 32.2km ambayo ilianza kujengwa mwaka 2017, imegharimu zaidi ya Sh52 bilioni mpaka kukamilika kwake.
“Kuhusu ubora ambao ulihitajika kimradi umetimizwa kwa kiwango cha juu na tulihakikisha vipimo vyote wakati wa ujenzi vilikua sashihi hivyo tunawahakikishia Watanzania katika barabara hii hatutapata tatizo kwa siku za karibuni mpaka umri wa barabara utakapofikia,tumefanya hivyo kulinda pesa za watanzania zilizowekezwa katika mradi wa barabara hii,” amesema Mhandisi Ntije.