Kigoma. Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano nchini Tanzania, Isack Kamwelwe amesaini mkataba wa ujenzi wa barabara ya Kabingo, Kasulu hadi Manyovu kwa kiwango cha lami.
Barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 260 itajengwa kwa miaka mitatu na kugharimu Sh340 bilioni.
Akizungumza kuhusu ujenzi huo leo Alhamisi Februari 21, 2020 mtendaji mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), Patrick Mfugale amesema mradi huo utachochea maendeleo na uwekezaji ndani na nje ya Tanzania.
Amesema kukamilika kwa mradi huo kutakuza biashara baina ya Tanzania na nchi za jirani zinazozunguka mkoa huo ikiwemo nchi ya Demokrasia ya Jamhuri ya Congo (DRC) na Burundi.
Barabara hizo zitakazounganisha wilaya za mkoa wa Kigoma, kupitia Kasulu hadi Manyovu Wilaya ya Buhigwe yenye urefu wa kilomita 68.25, Kanyani -Mvugwe wilayani Kasulu yenye urefu wa kilomita 70.5 , Mvungwe -Nduta wilayani Kibondo yenye urefu wa kilomita 59.35 na Nduta-Kibondo hadi Kabingo wilayani Kakonko yenye urefu wa kilomita 62.5.
Amesema mradi huo umefadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) kwa mkopo nafuu wa Sh340 bilioni.