Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Sh1.5 bilioni kujenga chuo cha Veta Wilayani Kwimba

65834 Chuo+pic.png

Sun, 7 Jul 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Kwimba. Serikali imetenga Sh1.5 bilioni kujenga Chuo cha Elimu ya Ufundi  (Veta) Wilaya ya Kwimba  mkoani Mwanza, Tanzania ili kuwasaidia vijana wapate ujuzi wa mambo mbalimbali, hatua itakayosaidia kukabiliana na ukosefu wa ajira na kuzurura mitaani.

Kauli hiyo imetolewa leo Jumamosi Julai 6, 2019 na Naibu Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha alipotembelea na kukagua  shughuli za uboreshaji wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi (FDC) Malya, wilayani hapa.

Amesema  lengo la Serikali ni kujenga vyuo vya ufundi katika wilaya 25 nchini, lengo likiwa ni kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa vijana.

“Fedha hizi tayari zimeshatengwa kwa ajili ya shughuli hiyo na lengo la Serikali ni kujenga vyuo hivyo katika wilaya 25 nchini, hii ni kwa ajili ya kuwajengea uwezo vijana wakapate ujuzi ambao utaweza kuwasaidia kwenye  maisha na kuongeza pato,” amesema.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Pendo Malebeja amesema tayari eneo limeshatengwa lakini wanakamilisha taratibu za umiliki wa hati kutoka kwenye halmashauri na kuwa kwenye miliki ya Veta.

Amesema, “Tumeshamaliza taratibu zote kilichobaki ni kujaza fomu za mikataba ambazo wakati wowote tunaweza kujaza. Naibu Waziri amewataka wafanye haraka kumaliza taratibu hizo ili ujenzi uanze mara moja.

Pia Soma

Kuhusu FDC, Naibu Waziri amesema Serikali imeanza kukarabati vyuo vyote 55  ili viweze kuwa na hali nzuri na wananchi waweze kupambana na kutawala mazingira yao kwa ajili ya kujiletea maendeleo.

Mkuu wa chuo cha Maendeleo Malya, Frank Josephat amesema wamepokea Sh445 milioni kwa ajili ya kujenga na kukarabati miundombinu ya chuo hicho, ambacho kwa mwaka huu wamedahili wanafunzi 138 lakini wanakabiliwa na changamoto ya vitendea kazi,  bweni na uhaba wa wakufunzi kwa ajili ya kutoa elimu inayostahili.

Chanzo: mwananchi.co.tz