Serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni 600 kwa ajili ya ujenzi wa mradi mkubwa wa maji wenye kisima na tenki lenye ujazo wa lita laki moja na nusu.
Akizungumza na wananchi katika Kata ya Dabalo Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Deogratius Ndejembi amesema hatua hiyo ni juhudi za serikali za kumtua mama ndoo kichwani.
"Niliahidi wakati wa kampeni zangu kwamba nitamaliza changamoto ya maji hapa Dabalo, hivyo niwaambie ujenzi huu wa kuchimba kisima na uwekwaji wa bomba umeanza kwa ajili ya kupeleka maji katika kisima ambacho kitakua na uwezo wa kuhifadhi maji,” amesema Ndejembi.
Aidha, amewashauri vijana wa bodaboda katika kata hiyo, kujiunga na vikundi ili aweze kuwaletea mafunzo ya kibiashara na kuwaunganisha na mabenki kwa ajili ya kupatiwa mikopo, pia kunufaika na mikopo inayotolewa na halmashauri.