Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Serikali ya Tanzania yaunda kamati ya kutatua migogoro ya wafugaji

Tue, 30 Apr 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dodoma. Serikali ya Tanzania imeunda kamati maalumu ambayo inatembea nchini kuhakikisha migogoro ya wafugaji na wakulima inapatiwa ufumbuzi.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega leo Jumanne Aprili 30, 2019 akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Mlalo (CCM), Rashid Shangazi.

Shangazi amesema katika eneo la wafugaji la Mkundi  tarafa ya Umba, kuna migogoro mara kadhaa.

“Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha sekta nzima ya ufugaji,” amehoji Shangazi.

Akijibu swali hilo, Ulega amesema Serikali imejipanga  katika kutatua na kwamba wameunda kamati inayotembea nchi nzima kuhakikisha migogoro ya wafugaji inapatiwa ufumbuzi.

“Napenda kumhakikishia wizara inayo mipango mizuri ya kuhakikisha fursa zinapatikana… majosho yamechukuliwa (Serikali) na yako katika mpango kuhakikisha yanaboreshwa na yakikamilika tutakuja kuzindua,” amesema.

Mbunge wa Chambani (CUF), Salim Yusuf Hussein  amehoji ni wapi kuna mfano wa eneo ambalo lina ufugaji bora na kilimo bora ambako watu wanaweza kwenda kujifunza.

Akijibu, Ulega amesema maeneo yapo mengi ya kujifunza na kutoa mfano wa Morogoro ambako kuna mfugaji mmoja anamiliki ng’ombe wa kisasa 700.

Naye Mbunge wa Monduli (CCM), Julius Kalanga amehoji   iwapo kuna mkakati wa upatikanaji wa mbegu bora ili kusaidia wafugaji.

Akijibu swali hilo, Ulega amesema Serikali ina mpango kabambe wa kuhakikisha wanaboresha kwa kusimamia mifugo na uvuvi.

Amesema Serikali ina mikakati mitatu ikiwemo ule wa kupitia madume bora yanayopatikana katika mashamba yao.



Chanzo: mwananchi.co.tz