Simanjiro. Watu saba wamefariki dunia na wengine 30 kujeruhiwa baada ya lori walilokuwa wamepanda kupinduka katika kijiji cha Namalulu wilayani Simanjiro mkoani Manyara.
Majeruhi saba walichukuliwa na ndege ndogo na kupelekwa Hospitali ya Seliani jijini Arusha, watano wamelazwa kituo cha afya Orkesumet na wengine walipatiwa matibabu na kuruhusiwa.
Akizungumza leo Jumatatu Septemba 9, 2019 kamanda wa polisi Mkoa wa Manyara, Agostino Senga amesema ajali hiyo imetokea leo saa 2 asubuhi.
Amesema imetokea barabara kuu ya Arusha-Orkesumet, kwamba lori hilo aina ya Fuso lilikuwa likitokea jijini Arusha kwenda mnadani wilayani Simanjiro.
Amesema chanzo cha ajali hiyo bado hakijajulikana, “Liliacha njia na kupinduka, watu watano walifariki dunia papo hapo na wengine wawili walifariki wakati wakipatiwa matibabu kwenye kituo cha afya Orkesumet.”
Amesema waliokufa ni Leapa Lekara (31), Aloyce Temba (32), Mosses Mgonja (31), Chemana Shedrack (36), Anna Kileo (46), “wengine wawili hawajatambulika.”
Pia Soma
- Lissu achambua uamuzi wa mahakama kukataa maombi yake, asema atakata rufaa
- Waziri Lukuvi azindua ulipaji kodi ya pango la ardhi kwa njia ya simu
- Tetemeko la ardhi lazua taharuki Katavi, watoto wawili wajeruhiwa