KATIBU Mkuu Wizara ya Maji, Anthony Sanga ameupa siku 60 Wakala wa Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (Ruwasa) kuhakikisha mradi wa maji wa Ilolo-Bulongwa unaanza kufanya kazi.
Aidha, amesema serikali itatoa Sh milioni 100 za awali wiki ijayo kwa ajili ya kuwezesha mradi huo kuanza.
Katibu Mkuu huyo alitoa agizo hilo mwishoni mwa wiki akiwa na Mbunge wa Makete, Festo Sanga, alipotembelea milima ya Kisajanilo kwa ajili ya kufuatilia chanzo cha mradi huo wa maji.
"Ninawaagiza Ruwasa ndani ya siku 60 mradi huu ukamilike, Jumanne (kesho) tutaleta Sh milioni 100 za kuanzia," alisema.
Alisema Mbunge wa jimbo hilo, Sanga amekuwa akimkumbusha kila mara kuhusu matatizo ya maji kwa wananchi wake ili waweze kupata maji safi na salama.
“Mbunge amenisumbua sana na nimefanya naye vikao zaidi ya mara tatu juu ya hali ya maji Makete, nilikuwa Shinyanga lakini nimetembea usiku kucha kufika Makete ili tushughulikie changamoto za maji," alisema.