Mbozi. Rais wa Tanzania, John Magufuli ameagiza wakazi wa kijiji cha Nanyala wilayani Mbozi mkoani Songwe kuendelea kulitumia eneo ka ukubwa wa ekari 2,115 linalogombewa na wakazi hao na kiwanda cha saruji Mbeya.
Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Oktoba 4, 2019 aliposimama katika kijiji hicho na kuelezwa kero hiyo na mwenyekiti wa kijiji hicho, Philmon Namwema.
Mwenyekiti huyo amesema mgogoro huo umedumu kwa muda mrefu na wamezuiwa kufanya shughuli yoyote, wananchi 23 wakikabiliwa na kesi mahakamani.
Akitoa uamuzi huo, Magufuli amewaagiza mawaziri kukaa pamoja na kufuta kesi iliyopo mahakamani na baada ya hapo wamjulishe ili aweze kubadili matumizi ya eneo hilo.