Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

RITA yatoa talaka 221 Dar

39148de3540b5b19ffb556009c01aee2 RITA yatoa talaka 221 Dar

Wed, 27 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

WAKALA wa Usajili, Ufilisi, na Udhamini (RITA) umetoa vyeti vya talaka 221 katika Mkoa wa Dar es Salaam baada ya wanandoa kuamua kuachana.

Akizungumza katika maonesho ya Wiki ya Sheria yanayoendelea kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam, Wakili Mwandamizi wa Serikali wa RITA, Edna Kamara alisema talaka hizo zilitolewa kuanzia Januari hadi Desemba mwaka jana.

Hata hivyo, alisema huenda idadi hiyo ingekuwa ya juu zaidi kama ndoa zote zinavunjika kisheria mahakamani, kimila au mazingira ya kawaida zingeweza kutolewa taarifa RITA kama taratibu zinavyowataka huku akisisitiza kuwa ni muhimu kwa wanandoa hao wanaoachana kufuata utaratibu huo ili kuepusha migogoro inayoweza kujitokeza.

“Tafiti mbalimbali zimeonyesha kumekuwa na idadi ya wanandoa wengi wanaoachana baada ya ndoa zao kuvunjika, hii imepelekea mahakama nyingi kuwa na kesi hizo huku idadi ndogo ya wanandoa hao wakifika katika ofisi yetu wakiwa na nakala ya hukumu iliyotolewa na mahakama kwa ajili ya kuhitaji vyeti vya talaka,” alisema Kamara.

Alisema hiyo ni changamoto ambayo wanandoa wanapaswa kuiangalia kwa jicho la karibu ili kupunguza kasi kubwa ya wao kuachana ambayo matokeo yake husababisha kuvunjika kwa mahusiano mazuri ya familia ikiwemo watoto, ndugu na jamaa wengine kuathirika.

Aliwataka wananchi ambao wamefikia hatma kisheria katika ndoa zao kujenga utamaduni wa kwenda kuandikisha talaka ili kupewa vyeti vitakavyowatambulisha kuwa wao ni watu huru ili kuepusha suala lolote linaloweza kujitokeza.

Alisema mbali na huduma hiyo, kupitia maonesho hayo ambayo kilele chake ni Februari Mosi, wanatoa huduma zingine mbalimbali zikiwemo za usajili wa vizazi na vifo,wosia, ufilisi na udhamini.

Chanzo: habarileo.co.tz