MKUU wa Mkoa wa Tabora, Dk Philemon Sengati, ametoa mwezi mmoja kwa Wakala wa Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira (Ruwasa) wilayani Nzega, kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama katika kijiji cha Ubinga ndani ya mwezi mmoja.
Alitoa agizo hilo jana wilayani Nzega baada ya kukuta mradi wa maji safi na salama katika kijiji cha Ubinga haujaanza kutoa huduma kwa wananchi licha ya kukamilika kwa asilimia 95.
Dk Sengati alisema mradi huo ambao umeigharimu serikali Sh milioni 460.6 ni lazima uanze kutoa huduma ya maji kwa wakazi wa kijiji hicho.
“Ni lazima wananchi wafaidi matunda ya serikali yao ikiwamo mradi hu una kuwaondolea adha ya kutafuta maji umbali mrefu na kuwakinga na magonjwa yanayotokana na matumizi ya maji yasiyosafi na salama,” alisema.
Kaimu Meneja wa Ruwasa Wilaya ya Nzega, Mhandisi Gaston Ntulo, alisema mradi huo umefikia asilimia 95 na kazi iliyobaki kwa sasa ni kuweka pampu itakayotumia nishati ya jua.
Alisema mradi huo utakapokamilika utawanufaisha wakazi 3,495 na kwamba utakuwa na tenki lenye ujazo wa lita 60, vituo vya kuchotea maji 12 na ulazaji wa bomba la mita 12,874 na kujenga sehemu kwa ajili ya mifugo kunywa maji umefanyika.
Mhandisi Ntulo alisema pamoja na mradi huo kukamilika, bado wanadaiwa na kampuni ya Monmar and Sons kwa kwani haijalipwa hata shilingi moja.