MKUU wa Mkoa wa Tabora Dk Philemon Sengati ameagiza matofali yaliyotumika kujenga nyumba ya mwalimu kwenye Shule ya Sekondari ya Kamagi yapimwe ubora wake.
Alitoa agizo hilo jana wakati wa ziara ya kukagua miradi ya maendeleo wilayani Sikonge.Dk Sengati alisema ni lazima wataalamu wapeleke matofali wawili maabara yachunguzwe kubaini ni kwa nini yanapukutika yanapoachiwa.
Alisema ikibainika tatizo ni matumizi madogo ya saruji atamuwajibisha mhandisi wa halmashauri na waliohusika kufyatua matofali hayo.
Dk Sengali alisema, hawezi kukubali kuona jengo limejengwa kwa shilingi milioni 14 lakini miongoni mwa matofali yanapukutika.
Alisema hali hiyo ni hatari kwa sababu inaweza kusababishai nyufa katika jengo mda mfupi baada ya kukamilika.
Dk Sengati aliwataka wote wanaopewa kazi ya kujenga miradi ya umma wazingatie vipimo vinavyokubalika kitaalamu ili miradi iwe na ubora unaokusudiwa.
Alisema hatasita kuwachukulia hatua wote ambao watasimamia miradi iliyo chini ya kiwango kilichopo kwenye mikataba.