Tabora. Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri amesema wameunda kikosi kazi maalumu cha kupambana na changamoto za uharibifu wa mazingira.
Mwanri ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Agosti 23, 2018 mbele ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba katika kongamano la kuhifadhi na kutunza mazingira kwa mkoa wa Tabora.
Mwanri aliyewahi kuwa Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi) amesema wamechukua uamuzi huo ili kukabiliana na changamoto mbalimbali za uharibifu mazingira mkoani humo.
"Hapa Tabora ingawa tunajitahidi lakini bado kuna uharibifu wa mazingira ikiwemo watu kuchoma miti na kuikata kinyume cha sheria,” amesema.
"Tatizo la mazingira hadi kuku anaijua. Mfano hapa manispaa mbuzi wanazurura ovyo mitaani na wanakula hadi ubwawa ulioungwa na nazi," amesema Mwanri na kusababisha watu kuangua kicheko.
Amesema kamati hiyo imewajumuisha watu mbalimbali wakiwemo walimu wakuu na wasaidizi wa shule za sekondari na msingi sambamba na wananchi na madereva bodaboda.
" Najua kuna watu hawachelewi kuwaambia nyie (kamati) ni nguvu ya soda, nawaambia mtasikia hadi maneno ya nguvu ya gongo lakini mkoa umejipanga ipasavyo kupambana na uharibifu wa mazingira,"amesema Mwanri.
Mwanri amefafanua kuwa kikosi kazi hicho, kimeundwa kuanzia ngazi ya vijiji, vitongoji, mitaa, wilaya hadi Mkoa.
Kwa upande wake, Makamba amesema ofisi yake inatambua jitihada za Mkoa huo kupambana na uharibifu wa mazingira, kubainisha kuwa unakabiliwa na changamoto za uhifadhi wa mazingira ikiwemo kilimo cha tumbaku, ukataji wa miti na ufugaji holela.
"Makamu wa Rais anatambua kazi kubwa mnayoifanya ndio maana ametuma nije huku tena. Pia nimekuja kutizama orodha ya maeneo mnayotaka tuyape ulinzi kwa mustakabali wa Taifa," amesema Makamba.