Mtwara. Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Gelasius Byakanwa amewataka wakulima wa korosho mkoani humo kuwatumia wataalamu wa kilimo ili kuzalisha zao hilo kwa wingi.
Akifungua mafunzo ya matumizi sahihi ya viuatilifu kwa baadhi ya wakulima wa korosho katika kijiji cha Mailikumi leo Jumatano Juni 12, 2019, Byakanwa amesema Mikoa mingine inayolima korosho inazingatia ushauri wa wataalamu.
“Tunavyojisifu kwa kilimo cha korosho kwamba ni wazalishaji wakubwa tutambue mikoa mingine imeanza kulima zao hili. Tukiendelea kubweteka wakati wenzetu wanalima kisasa na wana matumizi sahihi ya viuatilifu tutajikuta tunakuwa nyuma katika uzalishaji.”
“Zaidi ya asilima 60 ya korosho inatoka Mtwara ikifuatiwa na Lindi na Ruvuma, mikoa mingine wana maeneo mengi ya kulima na pengine kutumia mbegu za kisasa zilizotokana na utafiti wa chuo cha Naliendele. Chonde chonde wana Mtwara tubadilike siku za usoni takwimu zinaweza kubadilika mkajikuta nyie ni wa mwisho,” amesema Byakanwa
Kaimu mkurugenzi mkuu wa bodi ya korosho, Francis Alfred amesema “Katika tasnia ya korosho tunaangalia kuanzia uzalishaji mpaka masoko, kwa kipindi cha miaka miwili iliyopita kuanzia 2017/18 uzalishaji ulipanda na kuwa tani 313,000 lakini 2018/19 uzalishaji ni tani 244,000.”