Moshi. Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira amesema njia pekee ya kuwaondoa tembo waliovamia makazi ya watu ni kutumia nyuki.
Ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Agosti 31, 2019 wakati akikagua mizinga zaidi ya 50 ya nyuki aliyoagiza itengenezwe katika Chuo cha Viwanda vya Misitu Tanzania (Fiti) kwa ajili ya kudhibiti wanyama pori hao.
"Lengo ni kuweka mizinga ya nyuki kwenye njia wanazopita tembo, hiyo ndio njia pekee ya kuwarudisha katika hifadhi maana wanaogopa sana nyuki.”
"Tembo ni wengi kwenye makazi ya watu na wamefanya uharibifu kwenye maeneo mengi ya wananchi ikiwemo kuharibu mazao na kuua, kama Mkoa tumeona ni vyema tukakabiliana nao kwa namna hiyo," amesema Mghwira
Amebainisha kuwa maeneo mengi yanayovamiwa na tembo yapo katika maeneo ambayo wanyama hao hupita.
Mwenyekiti wa kitongoji cha Igoma, Julius Mtegwa amesema kwa miaka mingi tembo hao wamekuwa wakivamia mashamba ya wananchi na kufanya uharibifu wa mazao ikiwemo mahindi na mihogo, kwamba zaidi ya ekari 50 za mazao ziliharibiwa mwezi Juni, 2019.