Mbeya. Mkuu mpya wa mkoa wa Mbeya, Albert Chalamilla amekabidhiwa ofisi na aliyekuwa mkuu wa mkoa huo, Amos Makalla na kuahidi kuanza na kushuka kwa mapato ya jiji la Mbeya.
Akizungumza leo Jumatatu Agosti 6, 2018 baada ya kukabidhiwa nyaraka mbalimbali, Chalamilla amesema wakati wakiapishwa na Rais John Magufuli, alitaja kushuka kwa mapato ya jiji hilo, jambo ambalo lilimuingia vilivyo.
“Siku ile Mbeya ilitajwa na Rais jinsi inavyolegalega katika ukusanyaji mapato. Lazima tuketi kwa pamoja na tutafakari usahihi wa hoja hiyo, kujua njia sahihi za kukabiliana na hali hii,” amesema.
“Ukiona mkuu wa nchi anazungumzia masuala ya kodi wakati kodi ndio haswa zinazosukuma na kuliendesha Taifa lazima tukae pamoja tujidhatiti ili tuwe miongoni mwa majiji yenye ukusanyaji bora wa mapato,” amesema.
Amesema yeye si mtu wa kuyumbishwa na mtu yeyote katika utendaji wake wa kazi ana ametaka aachwe atekeleze majukumu aliyopewa na Rais kwa wananchi wa Mbeya.
Kwa upande wake Makalla amesema akiwa katika mkoa huo alisaidiana na watu mbalimbali na kumtaka Chalamilla kusimamia mambo ambayo alishindwa kuyakamilisha na yale aliyoanza kuyatekeleza.
Makabidhiano hayo yalienda sambamba na kuapishwa kwa mkuu mpya wa wilaya ya Chunya, Maryprisca Mahundi ambaye baada ya kuapishwa amesema si kiongozi wa kuwekwa mfukoni na mtu.