Mbarali. Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Albart Chalamila amesema ni fedheha na aibu kwa madiwani kuingia kwenye vikao vya kujadili maendeleo ya halmashauri zao huku wakiwa na mihemko ya itikadi za siasa za vyama vyao.
Amesema vyama vya siasa si ugomvi, kwamba Chama cha Mapinduzi (CCM) na viongozi wake wana wajibu wa kupokea ushauri wote mzuri kutoka upinzani na kuufanyia kazi kwa ajili ya maendeleo ya Mkoa huo na sio kubeza.
Ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Agosti 18, 2018 mjini Rujewa kwenye kikao maalumu cha baraza la madiwani la halmashauri ya Wilaya ya Mbarali kilichoketi kwa ajili ya kujibu hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Amewataka madiwani wa Mkoa wa Mbeya kuacha tabia ya kusongwa na mihemko ya kisiasa ambayo hazisaidii maendeleo ya halmashauri na kata wananaziongoza.
Amesema kuendekeza siasa za aina hiyo kunadhoofisha ukuaji wa uchumi wa Mkoa huo na wananchi wake.
Amebainisha kuwa anakaribisha maoni na atayapokea bila ubaguzi, kusisitiza kwamba atakayepekea maoni hayo ahakikishe yawe ya kujenga na si majungu.
“Kwa lugha nyepesi mnapongia hapa ndani kwa ajili ya kujadili mustakabali wa halmashauri hii (Mbarali) ni kitendo cha fedheha kama mtaingia mkiwa na mihemko ya itikadi ya vyama vya kisiasa,” amesema.
“Narudia tena ili tuijenge Mbarali na Mbeya yetu, madiwani wa Chadema na wa CCM mnaitwa madiwani wa Serikali ya Tanzania na wajibu wenu ni mmoja tu kuwawakilisha wananchi kwa hoja imara na kuisimamia Serikali yenu iweze kufanya vitu vyake vizuri.”