Makalla amesema hayo baada ya kukutana na wazee hao, huku akisema kuwa anatambua thamani na mchango wa Wazee katika jamii hivyo ameona ni vyema kuanza majukumu yake kwa kukutana nao kwani Wazee ni hazina muhimu.
Aidha, amesema katika kutatua kero na changamoto za Wananchi amepanga kuanza ziara ya utatuzi Kata kwa Kata hivyo amewahakikishia wananchi kuwa anayo dhamira ya dhati ya kupata majibu ya kero zao.
Hata hivyo Makalla amesema kwa kuwa Mkoa wa Dar es salaam ni Mkoa mkubwa na wenye kutoa taswira ya nchi nzima kwenye kila nyanja mbalimbali, amejipanga kuhakikisha Jiji linakuwa shwari na watu wanafanya shughuli zao bila usumbufu wowote, kama maono na mategemeo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.
Kwa upande wao Wazee walioshiriki katika kikao hicho wamemshukuru na kumpongeza Mkuu wa Mkoa huyo kwa namna anavyoheshimu Wazee na wamemuahidi kumpatia ushirikiano wa kutosha katika majukumu yake.