Dodoma. Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk Binilith Mahenge ameiomba Serikali ya Tanzania kuregeza masharti ya kodi kwa wawekezaji hasa katika mkoa huo.
Ametoa kauli hiyo leo Jumatano Februari 12, 2020 wakati akimkaribisha Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Angellah Kairuki katika kongamano la sita la wadau wa kilimo, mifugo na uvuvi.
Mkuu huyo wa Mkoa amesema masharti magumu ya uwekezaji si rafiki kwa kuwa mkoa huo ni wa kimkakati.
"Tunaomba kuwe na masharti rafiki na vikwazo vipunguzwe kwani haviwi rafiki kwa wawekezaji wetu," amesema Mahenge.
Dk Mahenge amesema masharti hayo yanaweza kulegezwa kwa kipindi maalumu katika maeneo maalum.
Pia amewataka Watanzania kujenga utamaduni wa kupenda bidhaa zinazozalishwa nchini ili kuinua uchumi wa Taifa.