Iringa. Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Ally Hapi amesitisha likizo za wakuu wa Wilaya na wakurugenzi wa halmashauri mkoani humo huku akiwataka kutosafiri nje ya Mkoa huo baada ya kufanya vibaya katika ugawaji wa vitambulisho vya wafanyabiashara wadogo.
Hapi ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Mei 27, 2019 wakati akizungumza na watendaji wa halmashauri na kuwapa muda wa wiki tatu kuhakikisha wafanyabiashara wote wanapata vitambulisho hivyo.
Amebainisha lengo la Rais John Magufuli aliyegawa vitambulisho hivyo kwa wakuu wa Mikoa wote nchini ni kutaka wafanyabiashara wanatambuliwa na kuchangia maendeleo ya nchi kwa kulipa kodi.
Amewaonya watendaji wa vijiji na Serikali wanaodai kuwa vitambulisho vinasababisha mapato kupungua, akidai kuwa hiyo ni hoja dhaifu.
Hapi ameanisha makundi 53 ambayo yanastahili kupata vitambulisho hivyo, wakiwemo waandishi wa habari, wapiga debe, wauza mahindi, mchicha.
Amesema hakujiandaa kushindwa katika ugawaji wa vitambulisho na ndio sababu ya kusitisha likizo za viongozi hao ili wagawe vitambulisho hivyo ndani ya muda aliouweka ili Mkoa huo uweze kushika nafasi ya tatu katika ugawaji huo.
Pia Soma
- MADAI: DPP awatuhumu wabunge kwa rushwa, Spika ajibu
- Wafanyabiashara walia bei ya mifuko mbadala
- Hukumu kesi ya Lucky Vincent kusomwa kesho