Iringa. Mkuu wa mkoa wa Iringa (RC) nchini Tanzania, Ally Hapi amesema kuanzia Septemba 20 hadi 22, 2019 kumbi za burudani na hoteli mkoani humo zitafanya kazi saa 24 kuhakikisha wageni wanaofika mkoani hapo katika maonyesho ya utalii wanapata huduma muda wote.
Hapi amesema hayo leo Jumatatu Septemba 16, 2019 wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na maonyesho ya utalii ya karibu kusini.
Amesema maonyesho hayo yanatarajiwa kuzinduliwa Septemba 20, 2019 na Rais wa Zanzibar, Ali Mohamed Shein katika viwanja vya Kihesa Kololo mkoani humo.
Hapi anawakaribisha wananchi, watalii na wawekezaji kuona mipango na fursa zilizopo katika utalii wa Nyanda za juu Kusini.
"Fursa hii ni kubwa na ndio fursa pekee ya kuhakikisha tunaonyesha jinsi Iringa ilivyojipanga kupokea miradi mikubwa ya utalii," amesema