Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

RC Gambo ajutia kuwaweka rumande watumishi

85660 Pic+gambo RC Gambo ajutia kuwaweka rumande watumishi

Sun, 24 Nov 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Arusha. Mkuu wa Mkoa wa Arusha nchini Tanzania (RC), Mrisho Gambo ameeleza kujutia hatua za kuwaweka rumande watumishi wa umma bila kuwasikiliza.

Leo Jumapili Novemba 24, 2019 Gambo kupitia ukurasa wake wa Instagram na baadae kuzungumza na Mwananchi amesema watu wasione siku hizi hawaweki watumishi ndani wakadhani hana mamlaka hapana kwani ametambua kuwa elimu haina mwisho na amekubali kujifunza.

"Nimeamua kujikosoa pamoja na kufanyia kazi maoni ya wanaonikosoa, sisi viongozi vijana bado ni wanafunzi wa uongozi, kila siku tunajifunza na kupata uzoefu, hakika uzoefu ni mwalimu mzuri," amesema Gambo alipozungumza na Mwananchi

Katika ukarasa wake wa Instagram Gambo amekumbushi alipokuwa Mkuu wa wilaya ya Uvinza mwaka 2015/16 akisema alimuelekeza mkurugenzi amuandalie kikao cha haraka cha watendaji wa Kata na vijiji.

Amesema kwenye kikao hicho ofisa mtendaji kata ya Itebula alichelewa kufika kikaoni na bila kumsikiliza alielekeza awekwe ndani saa 24.

"Kama ilivyo kawaida kesho yake nikaagiza aletwe ofisini kwangu kwa ajili ya utetezi, mtumishi yule alipofika ofisini alianza kujitetea kwa kuniambia , Mkuu wakati napata wito wa kikao chako nilikuwa hospitali na mke wangu, aliyekuwa mjamzito alikuwa na matatizo ya mimba.”

“Muda ule alipopokea wito alikuwa chumba cha upasuaji kwa kuheshimu wito wako Mkuu nilimwacha mke wangu hospitali nikakimbia kuja kwako nilidhani nikifika utanipa pole na kuona nimeheshimu wito wako badala yake ukaniweka ndani leo nimepata taarifa kuwa hali ya mke wangu na mtoto aliyeko tumboni ni mbaya zaidi,” anaeleza Gambo

Gambo alimnukuu ofisa mtendaji huyo kuwa, alimweleza tukio hilo hatalisahau kwenye maisha yake na anadhani alinyanyaswa na kuonewa kwa unyonge wake, hakika hapa umetumia ubabe na madaraka yako vibaya kwa hakika nilitamani kulia nilijisikia vibaya sana.

Katika maelezo yake hayo, Gambo anasema, “Kisa hiki cha kweli kilinifanya niache mchezo wa kuwaweka ndani watumishi. Nikaona haja ya kuwasikiliza watumishi kabla ya kuwahukumu. Kweli uzoefu ni mwalimu mzuri.”

Mwananchi lilimtafuta Gambo kutaka kujua alimwomba radhi mtendaji huyo na kuchukua hatua gani zaidi, amesema alimuomba radhi mtumishi huyo na kumrudishia nauli pamoja na mwenzie wa kijiji cha Sibwesa Kata ya Kalya.

Amesema watumishi ni binaadamu wana changamoto nyingi kama binaadamu wengine busara ni kuwapa fursa ya kujitetea kabla ya kuwahukumu.

"Hekima ni kushughulikia changamoto zao kwa kufuata kanuni za utumishi wa umma, kupitia kanuni za utumishi watapata wasaha wa kujieleza kabla ya kuchukuliwa hatua za kinidhamu na za kisheria," amesema.

Chanzo: mwananchi.co.tz