Karatu. Mkuu wa mkoa wa Arusha (RC) nchini Tanzania, Mrisho Gambo ameagiza kukamatwa viongozi na wanachama wote waliofilisi Chama cha Ushirika wa kuweka na kukopa (SACCOs) vya Ayalabe wilayani Karatu mkoani Arusha
Gambo ametoa agizo hilo leo Alhamisi Agosti 29,2019 wilayani Karatu katika ziara inayoendelea kukagua miradi ya wananchi na kusikiliza kero.
Amesema baadhi ya wanachama wa SACCOs hiyo wajumbe wa Bodi na kampuni mbili wanatuhumiwa kwa upotevu wa Sh520.6 milioni.
Mkuu huyo wa mkoa amesema mgogoro huo limechukua muda mrefu hivyo kumtaka kamanda wa polisi mkoa Arusha, Jonathan Shana uwakamate watuhumiwa wote wakati anafanya mawasiliano na ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali.
Ayalabe SACCO'S ilikuwa moja ya chama cha ushirika cha mfano mkoa wa Arusha baada ya kufanikiwa kuanzisha kiwanda cha kisasa cha maziwa lakini sasa kimesitisha uzalishaji.