Mbeya. Mkuu wa mkoa wa Mbeya, Albert Chalamila ametoa siku tatu kuanzia leo kwa watumishi wa Serikali wanaomiliki vibanda vya biashara jijini Mbeya kujisalimisha kwa wakurugenzi wa halmashauri kabla ya hatua kali kuchukuliwa dhidi yao.
Hayo ameyasema leo jijini hapa katika mkutano wake wa kujitambulisha kwa watumishi wa umma wa Halmashauri ya wilaya ya Mbeya na Jiji la Mbeya pamoja na watumishi wa taasisi mbalimbali zinazohusika na kuhudumia wananchi.
Chalamila amesema wapo baadhi ya watumishi wanaomiliki vibada na kuwapangisha wananchi wengine nakulipwa kiasi kikubwa cha fedha ambacho hakilipiwi kodi ipasavyo.
Amesema orodha kamili ya watumishi hao anayo japo hayuko radhi kuitaja mpaka pale watakapo kaidi kujisalimisha.
Pia amebainisha kuwa iwapo hawatojisalimisha adhabu kali ikiwamo kufukuzwa kazi kufikishwa mahakamani pamoja na kulipa fedha zote walizopokea kwa waliowapangisha zitawakabili.