Mkuu wa Mkoa wa Kagera Albert Chalamila amesema pamoja na wilaya ya Kyerwa kuzalisha kwa wingi zao la kahawa, bado ipo nyuma kimaendeleo kutokana na usaliti unaofanywa na baadhi ya wananchi, viongozi na watumishi wa serikali, kwa kuhusika na biashara ya magendo ya Kahawa kwenda nje ya nchi
Akizungumza na wananchi, viongozi na watumishi wa serikali wakati wa ziara yake aliyoifanya katika maeneo mbalimbali ya wilaya ya Kyerwa ikiwamo ya Murongo na Nkwenda, Chalamila amesema kuwa anawafahamu hata kwa majina viongozi wa Halmashauri, wa chama, Askari, mgambo na hata wananchi ambao wanahusika katika usaliti huo, na kwamba atakabidhi orodha hiyo kwa mamlaka zinazohusika ili uchunguzi uanze mara moja.
Amesema serikali ya mkoa haiwezi kuendelea kumuomba fedha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya kuboresha huduma ikiwamo barabara, wakati wanaruhusu Kahawa zitoke kwa magendo