Mbeya. Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Albert Chalamila amesema Mkoa huo uko mbioni kuanzisha operesheni maalum ya kutokomeza vibaka aliyoiita ‘operesheni ondoa vibaka’.
Ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Agosti 31, 2019 katika kikao na wadau mbalimbali wilayani Mbarali kujadili changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo na kuzipatia ufumbuzi.
"Tunaanza operesheni ondoa vibaka ili mji uwe salama na kama tutawahifadhi vibaka hao polisi au mahakamani sawa," amesema.
Chalamila ameitaka jamii kuwa sehemu ya ulinzi badala ya kuwaachia polisi pekee ili amani iendelee kutawala.
Akizungumzia shutuma anazorushiwa mitandaoni kuhusu kauli yake inayodaiwa kutozingatiwa haki za binadamu alipowataka wananchi kuchukua sheria mkononi, amesema hakuna mahali sheria inasema kuna haki ya vibaka.