Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

RC Ally Hapi atema checheTsh Bilioni 12/- za madarasa

D75a12380ea6c846fabe17eee1774d0a RC Ally Hapi atema checheTsh Bilioni 12/- za madarasa

Thu, 21 Oct 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

MKUU wa Mkoa wa Mara, Ally Hapi amesema Sh bilioni 12.3 walizopokea kwa ajili ya ujenzi wa madarasa zisitumike kulipa posho kwa wajumbe wa kamati za usimamizi na ufuatiliaji.

Hapi alisema mjini Musoma kuwa halmashauri zinapaswa kutumia vyanzo vyake vya ndani kwa ajili ya posho hizo na pia maeneo itakapojengwa miradi yasiwe yenye kuhitaji malipo ya fidia.

Aliagiza pia kuwa, maeneo hayo yasiwe na migogoro na kama kuna changamoto hizo halmashauri zisitekeleze miradi huko.

Alitoa maagizo hayo wakati wa mkutano wa uongozi wa mkoa huo na maofisa tarafa, viongozi na wataalamu kutoka wilaya na halmashauri zote za mkoa huo kujipanga kuhusu namna ya kutekeleza miradi hiyo ndani ya muda uliopangwa.

Mkutano huo ulifanyika katika ukumbi wa mikutano wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa ukiongozwa na Hapi akishirikiana na Katibu Tawala wa Mkoa huo, Albert Msovela.

Wajumbe walielezwa kuwa mkoa huo umepokea Sh bilioni 12.3 zitakazomaliza upungufu wa madarasa katika shule za sekondari na hadi Desemba 15 mwaka huu madarasa mapya 618 yawe yamejengwa.

Fedha hizo kutoka serikali kuu ni sehemu ya mkopo wa masharti nafuu wa Sh trilioni 1.3 kutoka kwa Shirika la Fedha Duniani (IMF) kwa ajili ya Kampeni ya Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya Covid-19.

Hapi alisema fedha hizo zimepokewa zikiwa na maelekezo mahususi kutoka kwa Rais Samia Suluhu Hassan ikiwa ni pamoja na muda, aina ya mfumo wa ununuzi wa vifaa na namna ya kuzitumia.

Alisema kwa mujibu wa maelekezo hayo fedha hizo ni kwa ajili ya ujenzi wa madarasa mapya tu si kwa ajlii ya kumalizia maboma ya madarasa ambayo ujenzi wake ulianzishwa na wananchi.

Hakuna mtu wala mamlaka itakayobadili matumizi ya fedha hizi au kuzidokoa, endapo itatokea serikali haitakuwa na huruma kwa atakayehusika,ยป alionya.

Serikali imeelekeza ununuzi wa vifaa ufanywe kwa pamoja na kwa utaratibu usiohusisha mlolongo wa uzabuni ili pamoja na mambo mengine, miradi itekelezwe ndani ya muda uliopangwa.

Mara imeunda Kamati ya Usimamizi na Ufuatiliaji ambayo Mwenyekiti wake ni Mkuu wa Mkoa, Makamu Mwenyekiti ni Katibu Tawala wa Mkoa na wajumbe kadhaa, wengi wakitoka Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa.

RC Hapi alisema Mkoa huo umejipangia hadi Desemba 15 ujenzi wa madarasa yote uwe umekamilika.

Mkutano uliafikiana madarasa yatakayojengwa yawekwe milango ya mbao ngumu na madirisha ya alminium.

Chanzo: www.habarileo.co.tz