Arusha. Polisi Mkoa wa Arusha wamewaua watu watano kwa madai kuwa ni majambazi.
Watu hao wameuawa kwa kupigwa risasi katika njia panda ya Matevez kata ya Olmot halmashauri ya Jiji la Arusha jana usiku Jumatano Januari 28, 2020.
Akizungumza leo Alhamisi Januari 30, 2020 Kamanda wa Polisi mkoani Arusha, Jonathan Shana amesema watu hao walikuwa wamepanga kufanya uhalifu Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara na walikutwa na pikipiki tatu.
"Baada ya kupata taarifa zao tulitumia kikosi kabambe na jasiri chenye ukakamavu na weledi wa hali ya juu kuweka mtego katika njia panda hiyo," amesema
Amesema usiku waliona pikipiki hizo na kuwataka kusimama walitii lakini baada ya muda walianza kufyatua risasi wakiwalenga polisi katika tukio lililodumu kwa dakika 35.
“Wanne walifariki hapohapo na mmoja aligeuza pikipiki na kukimbia lakini alipofika umbali kama wa mita 500 alipigwa risasi.”
Pia Soma
- Miili waliosombwa na maji yazua taharuki wilayani Serengeti
- CCM kumhoji Kangi Lugola
- Mtazamo wa wananchi Maalim Seif kuutaka uwenyekiti ACT-Wazalendo
"Eneo lile kulikuwa na bunduki moja aina ya shortgun pump action , bastola aina ya Chinese iliyofutwa namba za usajili, magazine mbili za bastola hiyo na risasi nane. Pia kulikuwa na maganda saba ya risasi ya bastola ya chinese, risasi mbili za bunduki aina ya shortgun na maganda matano ya risasi pamoja na simu mbili,” amesema kamanda huyo.
Amesema uchunguzi wa awali umeonyesha kuwa bunduki hiyo iliibiwa Januari 26, 2020 nyumbani kwa Jackson Msangi baada ya watu hao kuvamia nyumbani kwake.