Mwanza. Wakati baadhi ya wanawake wakihaha kupata watoto, wengine waliopata bahati hiyo huchukua uamuzi wa kuwatelekeza watoto wao na kutokomea kusikojulikana.
Jana Jumatatu Desemba 17, 2018 mwanamke mmoja amejifungua mtoto na kumtupa katika uwanja uliopo mtaa wa Mwambani wilayani Ilemela jijini Mwanza.
Akizungumza na wanahabari leo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Jonathan Shanna amesema kichanga hicho kinakadiriwa kuwa na umri wa siku moja hadi tatu.
Amesema wananchi waliomuona mtoto huyo walitoa taarifa polisi.
“Ilikuwa saa 2:30 usiku. Tulipata taarifa za kuwepo kwa mtoto huyo na tulipofuatilia tulimkuta akiwa amefunikwa na nguo na kutelekezwa katika uwanja. Alikuwa hai na alikuwa akilia sana,” amesema.
Amesema mtoto huyo alikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando na hadi kwamba anaendelea vizuri.
Amesema polisi wanaendelea na upelelezi wa kumsaka aliyemtupa mtoto huyo ili achukuliwe hatua, kuwataka wananchi wanaoishi na mwanamke ambaye alikuwa mjamzito na sasa hana ujauzito wala mtoto kutoa taarifa polisi.