Musoma. Jeshi la polisi mkoani Mara limemuua kwa kumpiga risasi mtu mmoja anayetuhumiwa kuwa ni jambazi alipojaribu kutoroka akiwa chini ya ulinzi wa polisi.
Akizungumza leo Juni 29, Kamanda wa polisi mkoa wa Mara, Juma Ndaki amesema jambazi huyo, Otiende Chacha (29) aliuawa kwa kupigwa risasi mbili kiunoni alipojaribu kuwatoroka askari wakati akiwapeleka kutambua alipoficha silaha.
Kamanda Ndaki amesema tukio hilo lilitokea jana usiku maeneo ya Stendi ya mabasi ya Bweri manispaa ya Musoma.
Imeelezwa, jambazi huyo alikamatwa na polisi akituhumiwa kuhusika katika matukio mbaimbali ya unyang’anyi wa kutumia silaha.
“Baada ya kumhoji mtuhumiwa alikiri kutekeleza vitendo hivyo na kwamba alikuwa akimiliki silaha mbili ambazo ni bastola na SMG,” amesema Ndaki.
Baadaye polisi walimchukua mtuhumiwa huyo kuwapeleka sehemu anakoficha silaha hizo.
Amesema wakati wanaenda eneo hilo ghafla alikurupuka na kuanza kukimbia kwa lengo la kutoroka ndipo askari walifyatua risasi hewani wakimtaka asimame lakini alikaidi hivyo kupigwa risasi mbili kiunoni hali iliyosababisha kutokwa damu nyingi na kufariki akiwa njiani kupelekwa hospitali.