Iringa. Wafanyabiashara wa vileo mkoani hapa wamelilalamikia jeshi la polisi kwa kuwapiga wateja na kuwakamata kabla ya muda wa kufunga huku wakiwalipisha faini.
Hata hivyo, kamanda wa polisi mkoa wa Iringa, Juma Bwire alisema taarifa za askari wake kupiga wateja wa baa alizipata juzi mchana baada ya kupigiwa simu na mkuu wa wilaya.
“Nimepata taarifa kutoka kwa (Richard) Kasesela kuwa kuna kundi la wafanyabiashara wa vileo wanalalamikia utendaji wa polisi, wamekubaliana kesho (leo) kufanya kikao cha pamoja natumaini tutatoa taarifa kamili ya kilichowasibu,” alisema Bwire.
Wafanyabiashara hao walitoa malalamiko yao juzi mbele ya Kasesela na kwamba takriban wiki tatu wamekuwa wakisumbuliwa na polisi wa doria kwa kuwapiga wateja na kuwataka walipe faini.
Mmiliki wa baa ya The Camillion, Happiness Matanji alisema utendaji wa polisi umegeuka kuwa vita nyakati za usiku wanapofanya doria kwenye baa, kwani huvamia maeneo hayo kabla ya muda wa kufunga na kuamuru wateja kukaa chini na kuanza kuwapiga wengine wakipelekwa kituoni.
“Nimelipia kibali cha kufanya biashara hiyo kuanzia saa 1:00 jioni hadi saa 9:00 usiku ili kuondoa usumbufu lakini naona hali imekuwa mbaya kutokana na polisi ambao huwacharaza wateja viboko kabla ya muda wa kufunga,” alisema
Pia Soma
- Dar es salaam ndiyo kwenye uamuzi wa mafanikio au kuangushwa
- Hoja ya Waziri Mpango kuhusu CCM ndiyo pekee yawagawa wananchi
- Maji ya moto kwa mama aliyejifungua hayana faida
Kasesela alikiri polisi kukosea na kuahidi kuongea na kamanda wa mkoa kufahamu kinachoendelea.
Alisema wafanyabiasara waendelee na biashara zao wakiwa huru.