Babati. Polisi Mkoani Manyara, wamejipanga kufanya doria ya magari na miguu ili kuhakikisha wananchi wa eneo hilo wanasherehekea sikukuu ya Pasaka kwa Amani bila bugudha.
Kamanda wa Polisi mkoani humo, Agostino Senga ameyasema hayo jana Jumamosi Aprili 20, 2019 alipokuwa akizungumzia mikakati ya ulinzi na usalama kwenye sherehe za pasaka.
Kamanda Senga amesema wanawahakikishia ulinzi na usalama wananchi wote wa mkoa huo na washerehekee kwa amani kwa sababu wamejipanga kufanya ulinzi kwenye maeneo mbalimbali.
Hata hivyo, amewataka wananchi kutoacha nyumba zao bila ulinzi, bali wajitahidi kuacha mtu mmoja alinde au kufunga milango ya nyumba zao kwa makini na wapeane taarifa na majirani zao.
“Tumejidhatiti kufanya ulinzi kwa doria ya magari na miguu katika barabara kuu zote za mkoa wa Manyara na tunawaasa wananchi kuwa ulinzi unaanza na wao wenyewe,” amesema kamanda Senga.
Amesema disko toto halitaruhusiwa mkoani humo ila kwenye maeneo ya wazi ikiwemo viwanja vya mpira hawakatazi kwa lengo la kuhakikisha usalama wa kutosha unakuwepo kwa watoto hao.
Ametoa wito kwa wanywaji pombe wawe tahadhari kwa kutoendeleza vyombo vya moto wakati wamelewa kwani watakuwa wanatembea na vifaa vya kupima kilevi barabara na watawachukulia hatua watakaowakuta wamelewa.