Nyumba yenye vyumba sita mali ya mfanyabiashara, Hamed Shamdini iliyopo Kata ya Kaloleni Manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro, imeteketea kwa moto huku lawama zikielekezwa kwa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoani humo kwa kushindwa kutoa msaada.
Moto huo uliozuka majira ya saa 1:20 asubuhi umedumu kwa zaidi ya saa moja kabla gari la Zimamoto kutoka kiwanda cha sukari cha TPC kufika kuuthibiti moto huo huku mali kadhaa zikitajwa kuteketea kwa moto.
Tukio hilo la moto ni la pili kutokea kwa mwezi wa Februari mwaka huu ambapo Februari 5, moto uliteketeza Soko la Mbuyuni huku kilio cha wananchi kikielekezwa tena kwa Jeshi la Zimamoto mkoani Kilimanjaro.
Mkuu wa Zimamoto Manispaa ya Moshi, Hasani Juma amesema wamekuwa wakishiriana na Zimamoto kutoka kiwanda cha sukari cha TPC kutokana na gari lao kuwa bovu.